Mwezi wa Desemba watu wengi ulimwenguni pote huona
picha za Yesu akiwa mtoto. Akiwa amelazwa kwenye hori, yaani, sanduku
kubwa linalotumiwa kulishia wanyama. Lakini je, tunapaswa kumkumbuka Yesu akiwa mtoto tu?— *
Acheni tuzungumzie njia muhimu zaidi ya kumkumbuka. Tunaweza kujifunza
kutokana na jambo lililowapata wachungaji waliokuwa malishoni karibu na
Bethlehemu usiku mmoja.
Ghafula malaika anawatokea wachungaji hao.
Anawaambia hivi: “Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” Pia,
malaika anawaambia watampata Yesu “akiwa amefungwa vitambaa na akiwa
amelala katika hori.” Papo hapo, malaika wengine wengi wanatokea na
kuanza ‘kumsifu Mungu.’
Ungehisije kama ungewasikia malaika wakimsifu Mungu?—
Wachungaji wanafurahi sana! Wanasema: “Na twende moja kwa moja mpaka
Bethlehemu tukaone jambo hili ambalo limetendeka.” Wanapofika huko
wanamkuta “Maria na vilevile Yosefu, na yule mtoto mchanga akiwa amelala
katika hori.”
Baadaye watu wengine wanakuja Bethlehemu ambako
Maria na Yosefu wanakaa. Wachungaji wanapowaambia kuhusu kilichotukia,
wote wanashangaa. Je, unafurahi kujua mambo hayo yenye kustaajabisha?—
Watu wanaompenda Mungu wanafurahi kuyajua. Sasa acheni tuone ni kwa
nini watu wanafurahi sana baada ya Yesu kuzaliwa. Ili tuelewe jambo
hilo, tutachunguza mambo yaliyotukia kabla Maria hajaolewa.
Siku moja malaika anayeitwa Gabrieli anamtembelea
Maria. Anamwahidi kwamba atazaa mtoto ambaye “atakuwa mkuu naye ataitwa
Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” Pia, Gabrieli anasema: “Atatawala akiwa mfalme . . . na ufalme wake hautakuwa na mwisho.”
Maria anataka kujua hilo litawezekanaje kwa kuwa
hajawahi kulala na mwanamume. Basi, Gabrieli anamfafanulia: “Nguvu za
Aliye Juu Zaidi zitakufunika,” na “kile kitakachozaliwa kitaitwa
kitakatifu, Mwana wa Mungu.” Huo ungekuwa muujiza mkubwa! Kuuhamisha
uhai wa Mwana wa Mungu kutoka mbinguni na kuuweka ndani ya tumbo la
uzazi la Maria.
Je, umewahi kuona picha zinazoonyesha wanaume watatu wenye hekima pamoja na wachungaji wakimtembelea mtoto Yesu?—
Ni jambo la kawaida kuona picha hizo wakati wa Krismasi. Lakini
hazionyeshi jambo sahihi. Wanaume hao watatu walikuwa wanajimu, walizoea
kufanya jambo ambalo Mungu alikataza. Acheni tuone kilichotukia
walipofika. Biblia inasema: “Walipoingia ndani ya ile nyumba wakamwona huyo mtoto mchanga pamoja
na Maria mama yake.” Wakati huo Yesu hakuwa mtoto aliyetoka tu kuzaliwa
ndani ya hori; bali alikuwa akiishi pamoja na Yosefu na Maria katika
nyumba!
Wanajimu walimpataje Yesu?—
Ile “nyota” haikuwaongoza kwenda Bethlehemu kwanza, bali iliwaelekeza
kwa Mfalme Herode huko Yerusalemu. Biblia inasema Herode alitaka kumpata
Yesu ili amuue. Sasa fikiria jambo hili. Unafikiri ni nani aliyetumia kitu kilichofanana na nyota kuwaongoza wale wanajimu kwa Herode?— Si Yehova, Mungu wa kweli, bali ni mpinzani na adui yake, Shetani Ibilisi!
Leo, Shetani anawafanya watu wamfikirie Yesu
kuwa mtoto aliyetoka tu kuzaliwa. Lakini Malaika Gabrieli alimwambia
hivi Maria: “[Yesu] atatawala akiwa mfalme . . . , na ufalme wake
hautakuwa na mwisho.” Sasa anatawala akiwa Mfalme huko mbinguni, na hivi
karibuni atawaangamiza adui wote wa Mungu. Hilo ndilo jambo tunalopaswa
kukumbuka kumhusu Yesu, na tunapaswa kuwaambia wengine kulihusu.
Soma Katika Bibilia Yako
- Luka 1:26-35; 2:8-18
- Mathayo 2:7-12; 1 Petro 5:8
- Ufunuo 19:19-21; 1 Yohana 2:17
No comments:
Post a Comment